info@ttcl.co.tz
+255 22 214 2000

TTCL QUEENS YAITOA JASHO CBE

Timu ya Mchezo wa Pete ya Shirika la Mawasiliano Tanzania –TTCL QUEENS imeifunga magoli 12 kwa 9 timu ya Wafanyakazi wa Chuo cha Elimu ya Biashara CBE katika mchezo uliochezwa Agosti 16 mwaka huu katika viwanja vya chuo hicho.

Mchezo huo ambao ulikuwa wa kirafiki timu ya CBE ndiyo ilitangulia kuziona nyavu za wapinzani wao hali iliyoamsha morali kwa timu ya TTCL kujituma Zaidi na kupata magoli kadhaa kabla ya mapumziko.

Hadi timu zinaenda mapumziko timu ya TTCL ilikuwa imefunga magoli 7 huku timu ya CBE ikiwa na magoli 4 ambapo kipindi cha pili TTCL iliongeza magoli 5 huku CBE ikiongeza magoli 5 pia.

Akizungumzia mchezo huo Bi. Getrude Kipengele amesema ulikuwa ni mchezo mzuri ambao umewapa fursa timu yake kujitathimi kuhusu hali ya mazoezi na uzoefu wa mchezo huo kuelekea maandalizi ya michuano ya SHIMIWI.

Bi. Kipengele amesema kuwa tangu kuanza kwa timu hii imekuwa ikionesha kuwa na mabadiliko chanya siku hadi siku na hivyo kuwajengea moyo wa kujiamini Zaidi na kuwa tayari kucheza na timu yoyote itakayokuja mbele yao.

“Timu yetu iko vizuri ndiyo maana tumeweza kuwashinda CBE na hii ni ishara njema kwetu yeyote atakayekuja mbele yetu tunamfunga tu” alisema Bi. Kipengele

Akizungumzia siri ya mafanikio waliyoyapata Bi Kipengele alisema kujituma, ushirikiano na upendo wakati wote wachezaji wanapohitajika kufanya mazoezi ndiyo imekuwa ngao yao na kuwafanya kuwa imara Zaidi.

Mbali na michezo kuwa nyenzo muhimu ya kuimarisha afya pia michezo ni fursa nzuri ya, kubadilishana mawazo na mitazamo ya masuala mbalimbali ya kuliletea Taifa maendeleo endelevu.